NAITWA ZAINABU ALIYU! Hii ni Hadithi ya Maisha yangu…..!!
Mimi ni Mtoto wa kwanza kati ya Watoto wanne, ni Mtoto wa kike wa pekee katika Familia yetu, ndugu zangu wengine wote ni Wanaume. Nimetokea katika familia masikini sana, lakini yenye Mama mwemye upendo sana japo hakusoma sababu Babu yangu hakuamini katika kusomesha Mtoto wa Kike, Mama yangu aliipenda sana Elimu na alitamani kutuona Watoto wake tukiipata elimu ambayo yeye aliikosa huko nyuma, Namshukuru Mungu nilikuwa Mtoto mzuri na mwenye adabu ambaye nilimfanya Mama yangu ajivunie.
Baba yangu hakuwa na utofauti na Baba wengine wa Afrika, aliipenda sana familia yake na alihakikisha tunapata mahitaji muhimu kama Chakula na mavazi, hakupenda nisome ila kwa ushawishi wa Mama alikubali niende shule, Baba yangu hakuwa na kazi nzuri sana alikuwa akifanya kazi ya kulima katika Mashamba, familia yetu ilijengwa katika misingi ya Uislam
Kutokana na hali yetu kimaisha, shuleni sikuwa na vitabu wala nguo nzuri za kuvaa lakini haikunifanya nikate tamaa nilipigania ndoto yangu ili siku moja nije kuwa daktari wa kwanza wa kike katika Mji wetu. Mji wetu haukuwa na huduma nzuri za maji, elimu hata Madawa, Watu walikuwa wakifa kwa kukosa huduma muhimu.
Nilikuwa na miaka 14 tu, lakini akili yangu ilikuwa ikiwaza mambo makubwa tofauti na umri wangu, siku zote niliziweka ndoto zangu mbele bila kujali wangapi walikuwa wakinicheka na kunisema vibaya, tulikuwa Wasichana wachache tu katika darasa letu sababu hakukuwa na mwamko mkubwa wa elimu, uwezo wangu darasani ulinifanya nipendwe sana na Waalimu, walinifanya Mimi kuwa wa mfano kwa Wanafunzi wengine huku Maisha yangu ya kukosa mahitaji yalifanywa kuwa funzo shuleni kwani sikuwa na vitu muhimu vya kujifunzia lakini nilikuwa nikifanya vizuri
“ZAINABU hana madaftari ya kutosha, hana Sare nzuri lakini anafanya vizuri, hii iwe funzo kwenu nyie wenye vitabu na mazingira mazuri, mkae chini mtafakari” Yalikuwa ni maneno ya Mwalimu Ibrahim ambayo mara nyingi alikuwa akiyarudia, maneno haya yaliwafanya wanafunzi wengi wa kike kunichukia na kuniona kama adui kwao, Mwanafunzi mmoja pekee aliyeitwa Aminata alinichukulia kama rafiki kwake, alinipenda na kunifanya nijione mwenye furaha shuleni.
Kipindi hicho tulikuwa tukijiandaa na mitihani ya kupanda darasa, siku moja nikiwa nyumbani najisomea alikuja Mjomba wangu aliyeitwa Suleiman, alikuja kumuona Baba akanikuta nikiwa najisomea akanitazama kisha akatikisa kichwa chake, nikamsikia akimwambia Baba kuwa
“Hee! bado unaendelea kumlisha msichana mkubwa kama huyu, unapoteza pesa na muda wako ili asome? huyu anapaswa kuolewa” Baba alimkata jicho kisha akasema kwa hasira
“Muache Mtoto asome, bado mdogo ndio kwanza ana miaka 14”
“Miaka 14 unasema nini wewe? Binti yangu ameolewa akiwa na miaka 13 tuu, unapoteza chakula bure” Alijibu Mjomba Suleiman bila woga wowote ule na kunifanya nijisikie vibaya sana, ndoto yangu ilikuwa ni kusoma na kutimiza malengo yangu niliyojiwekea.
Baba akamsogelea Mjomba Suleiman kisha akamuuliza “Hiki ndicho kilichokuleta hapa?”
“Aaah! hapana, nimekuja kuazima Reki yako nitairudisha kesho asubuhi” Baba hakujibu chochote akaenda kuchukua Reki akampatia, Mjomba aliondoka bila kuongeza neno lolote lile, nilijawa na faraja sana kuona Baba yangu ananipigania na kuhitaji kuniona nikifika mbali kielimu.
Katika Mji wetu ilikuwa ni kawaida sana Wazazi kuwaoza Binti zao wakiwa wadogo, nilimshukuru Mungu sababu Wazazi wangu hawakuwa kama Wazazi wengine wasio thamini elimu na haki ya Mtoto kusoma. Tulifanya Mtihani, nilifanya vizuri na kufaulu, ni Mimi na Aminata pekee ndio tuliofaulu kwa upande wa Wasichana, wengine wazazi wao walifanya jitihada za kuhonga kuhakikisha wanapanda darasa. Ilikuwa ni kawaida sana kuona Wazazi wanatumia pesa ili Watoto wafaulu.
Nilifika hatua kubwa ya elimu ambayo Wasichana hawakuwahi kufika katika Mji wetu, kwa muda mchache niliweza kuzungumza Kiingereza vizuri, hata Anko Suleiman alipokuja alinikuta nikizungumza Kiingereza vizuri
“Huna lolote unajifanya kuongea kiingereza ili uonekana ni Mtu mweupe?” Alisema lakini Baba alisimama upande wangu kitu ambacho kilimkasirisha sana Anko Suleiman.
Maisha yangu ya Shule yaliendelea japo Wasichana wengine walifanya niione shule chungu kwa maneno yao ya kejeri na dharau, tulipofunga shule nilibakia nyumbani kwa ajili ya kusubiria Mwaka ujao niweze kuingia kitado cha kwanza, Maisha yalianza kubadilika kwa upande wa Baba, alikosa kazi katika Mashamba, tulianza kuishi maisha magumu hata kula yetu ilikuwa ni mara moja tu kwa siku kitu ambacho kilimuumiza sana Baba yangu. Mdogo wangu Akeem alianza kuumwa, Mama alijitahidi kumpa dawa za mitishamba ambazo zilimsaidia kwa kiwango kidogo sana huku hali ikizidi kuwa mbaya, hofu ikatanda mioyoni mwetu kuwa Hakeem anaweza kufa muda wowote ule.
“Baba ni lazima tumpeleke Akeem Mjini kwa ajili ya Matibabu vinginevyo tunaweza kumpoteza” Nilisema kwa huzuni sana huku macho yangu yakitiririsha chozi lililobubujika hadi kwemye mashavu yangu
“Upo sahihi Zainabu lakini matibabu yanahitaji pesa na Mimi hapa sina pesa kabisa” Alijibu Baba kisha aliinamia chini
“Oooh Mungu msaidie Mwanangu apone” Ilisikika sauti ya Mama akiwa analia, kilikuwa ni kipindi kigumu sana
“Baba Zainabu kwanini usiende kukopa pesa kwa Alhaji Usman?” Mama aliuliza akiwa anajifuta mchozi, Alhaji Usman alikuwa tajiri sana katika Kijiji chetu, alikuwa akikopesha pesa.
“Huwezi amini Mke wangu nilisahau kabisa kuhusu hilo jambo, wacha niende mara moja” Alisema Baba kisha aliondoka haraka.
Yalipita masaa Matatu ndipo Baba aliporejea nyumbani lakini akionekana kutokuwa na furaha kabisa japo alipatiwa mkopo wa pesa, jambo hili lilitushangaza sana, Mama akamuuliza
“Baba Zainabu mbona unaonekana kama hauna raha kulikoni?”
“Amekubali kutupatia pesa lakini amesema tusimrudishie” Alisema Baba kwa Unyonge sana akiwa anakaa vizuri kwenye kiti
“Hizo ni Habari njema kwanini usifurahie?” Aliuliza tena Mama huku tabasamu likiwa limenijaa usoni pangu
“Anacho kihitaji ni kikubwa zaidi”
“Unasemaje? hakuna kitu kikubwa katika kupigania uhai wa Mtoto wetu”. Alisema Mama
“Amesema anataka kumuowa Zainabu” Baba alisema kisha moyo wangu ukawa kama umemwagiwa maji PWAAA, Nilihisi kulowa ndani ya moyo wangu
“Mungu zuia hili jambo” Mama alipaza sauti yake kisha alisimama, akaendelea kusema
“Mzee wa miaka 60 tena ana wake watano aje amuowe Binti yangu Zainabu? hilo haliwezekani kabisa”
“Hebu tulia Fatma Mke wangu, unajua nampenda sana Binti yangu lakini hakuna namna tunaweza kufanya, ameahidi kutupa pesa zaidi na kubadilisha Maisha yetu, tukubali tu ili Usman awe Mkwe wetu” Baba alisema , Nilibakiwa nikiwa nimepigwa bumbuwazi huku nikiwa nawatazama Wazazi wangu wakiendelea kurumbana kwasababu yangu kitu ambacho hakikuwahi kutokea, Nilistaajabu sana Kuona Baba yangu anaanza kulegeza msimamo wake aliokuwa akiukaza mwanzo kuwa nisome.
Hali ya Mdogo wangu ilizidi kuwa mbaya kitu ambacho kiliniogopesha sana, amani ya moyo wangu iliondoka sababu Mama na Baba hawakupatana kabisa, walinuniana kwasababu yangu, hali ngumu ya Maisha iliendelea kutupiga, njaa ilitumaliza nilitamani sana kuisaidia familia yangu hasa Akeem ambaye alikuwa mgonjwa huku akikosa chakula. Nilifikiria kuhusu elimu na ndoto zangu, sikutaka kabisa kupoteza muelekeo katika Maisha yangu tena kwa Mwanaume Mzee mwenye wake watano na watoto wakubwa walionizidi Umri, kila nililolifikiria niliona linaenda kunivunja moyo wangu lakini unafikiria ningefanyaje?
Siku moja Anko Suleiman alikuja nyumbani, namna sura yake ilivyo nilijua tu kulikuwa na tatizo, nilimsalimia
“Shikamoo Anko Suleiman” Hakujibu badala yake aliniuliza “Mama yako yupo wapi?”
“Yupo ndani ngoja nimuite” Niliinuka na kwenda kumuita Mama, siku hiyo Baba alikuwepo pia, walikaa na kuanza kuzungumza
“Fatma kwanini unataka kuiharibu hii Familia? kwanini wewe ni Mama Mbaya sana” Aliuliza Anko Suleiman
“Mimi sio Mama mbaya na siwezi kuiharibi Familia yangu mwenyewe, unasema nini Suleiman?” Mama alihoji
“funga bakuri lako, kwanza sikulaumu wewe kuwa hivyo bali namlaumu Mume wako aliyekupa mamlaka ya kuwa na sauti hapa
nyumbani, Fatma unang’ang’ania elimu ili ije kumsaidia nini Zainabu? unafikiri hata akisoma ndio hatoolewa?”
Nini Kitaendelea? USIKOSE SEHEMU YA PILI
SOMA RIWAYA YA FUNGATE KWA KUBONYEZA HAPA
SOMA RIWAYA YA NILIPANGA NYUMBA MOJA NA MAJINI
JIUNGE NIPO KIJIWENI Kwa Kubonyeza Hapa




1 Comment
Nice