Ilipoishia Nyumba Juu Ya Kaburi 08

Hakika nilikua katika nyakati ngumu zaidi kuwahi kupita kwenye maisha yangu. Hapakua na  yeyote pembeni yangu, nilipoinua macho baada ya kujifuta mchozi nilimwona Mama yangu  Mzazi kitu ambacho kilinishtua sana. Mtu ambaye tulimzika siku chache zilizopita alikua  amesimama mita kadhaa karibu na Bustani ya Mauwa. 

Alikua amevalia mavazi meupe kama ambavyo inasemekana Malaika huvalia, alikua msafi sana  kiasi kwamba alikua aking’aa mithiri ya Kioo juani, halafu alikua akitabasamu sana. Macho  yalinitoka nikimtazama Mama yangu, nilijua Mama yangu amerudi kunisaidia kwenye hii vita. Endelea

SEHEMU YA TISA

Palikua tulivu ghafla, hapakua na upepo wa aina yoyote ule. Nilitamani kusogea niongee na  Mama yangu pengine alihitaji kuzungumza na Mimi. Mama alinionesha ishara ya kumsogelea  anikumbatie 

“Mamaa‼” niliita kwa sauti ya chini, chozi nalo lilidondoka kwa kasi huku majonzi yakiwa  yametanda. Nilitembea taratibu kumuelekea Mama yangu huku nikimtazama sana, Mama  hakuacha kutabasamu. Nilisogea karibu zaidi, kila hatua ilizidi kunisogeza karibu naye na  kumtazama kwa makini zaidi, alikua ni Mama yangu kabisa 

Nilibakisha hatua chache kuelekea alipo, niliona nitachelewa pengine ataghaili na kuondoka,  nilipiga hatua iliyoambatana na mkimbio. Mazingira yalikua kama yameganda hivi, Dunia kama  ailikua imesimama hivi. 

Ghafla nililiona shimo kubwa ambalo hatua yangu ilikua ikilielekea shimo lile, hapakua tena na  Mama yangu isipokua Mimi kujiokoa nisitumbukie ndani ya shimo, niligundua ulikua mtego na  bahati nzuri niliweza kufunga breki ya haraka kiasi kwamba niliyumba huku nikijinasua,  hatimaye nilifanikiwa kutoingia ndani ya shimo lile. 

Mara nilianza kuisikia sauti ya Mama yangu akicheka kwa kutisha sana. Sauti yake ilikua  ikiniumiza masikio yangu kiasi kwamba nilihisi kizunguzungu, nilipepesuka kama mlevi.  Nikajishikiza ukutani hadi nikafika mlango wa kuingilia ndani. 

Ile sauti ilipotea, ukimya ulianza tena. Yaani palikua na hali tofauti tofauti kila hatua ninayoipiga,  mapigo ya moyo yalikua yakizisindikiza hatua zangu. Niliinua macho na kuziangalia ngazi  zinazoelekea juu, kisha nilishusha macho yangu kuelekea kwenye korido ambayo kile chumba  nilichoambiwa kilikua kinapatikana. 

Hapakua na sauti nyingine isipokua sauti ya kudunda kwa moyo wangu na sauti ya pumzi zangu  zilizokua zikitoka na kuingia bila mpangilio. Nilisimama nikifikiria nielekee wapi, kitu cha  kwanza nilitaka kua na uhakika kua lile jini halipo ndani ya nyumba. 

Mahali pekee ambapo ningeweza kua na uhakika ni kupitia dirisha la Chumbani kwangu,  nilipandisha ngazi kuelekea chumbani kwangu. Nilipofika, nilijipa sekunde kadhaa kabla ya 

kufunua pazia. Nyumba ya yule Mzee jirani ilikua kimya sana, nilikua najua fika kua ilikua  ikikaliwa na yule jini Mzee 

Ukimya bado uliendelea kutikisa nyumba nzima na nyumba jirani, niliwaza kwa haraka atakua  yupo wapi. Niliutazama mkono wangu wenye shanga ya Ulinzi, nilikua na uhakika kua  asingeliweza kunidhuru kwa mikono yake isipokua kwa akili na kutumia viumbe vingine kama  alivyofanya wakati ule alivyowatumia Wazazi wangu. 

Nilijiambia moyoni kua sipaswi kuamini chochote kile sababu unaweza kua mtego kama  alivyotaka kuninasa dakika chache zilizopita kupitia taswira ya Mama yangu. 

Kuishi ndani ya ile nyumba lilikua ni wazo lililogoma kukubaliwa na moyo wangu, nilipaswa  kuifanya kazi niliyoambiwa siku ya leo, kwakua sikumwona yule jini na palikua kimya sana,  niliona ni muda muafaka wa kwenda chumba cha chini kuitoa nafsi ya Sabra. 

Niliuelekea mlango taratibu, kwakua nilikua nimeufunga nililazimika kuufungua ndipo nitoke  chumbani kwangu, palikua tulivu sana kiasi kwamba kila hatua yangu niliisikia vyema. Sauti ya  Bawaba za mlango zilipiga kelele wakati naufungua mlango, nilishupaza shingo yangu na  kuminya macho yangu huku nikiendelea kuufungua mlango kwa adabu sana. 

Nilipomaliza kuufungua Mlango, zoezi la kutoka chumbani lilianza taratibu, nilishusha ngazi  baada ya kuimaliza korido fupi kutoka chumbani kwangu. Nilitembea taratibu na kwa tahadhari  kubwa, nilipofika ngazi ya mwisho nilianza kuisikia ile sauti ya Mwanamke anayeimba. 

Alikua akiimba kwa masikitiko sana japo sikuitambua lugha yake ila sauti yake ilinifanya nihisi  masikitiko yake, nilisimama nikiendelea kuisikia huku nikifikiria nini cha kufanya, nilisimama  kwa dakika kama mbili hivi nikiendelea kutafakari, mwisho niliamua kuifuata ile sauti. Hapo  moyo wangu ulikua umekufa kwa woga, mwili wangu ulikua hauna nguvu, nilikua natetemeka  sana. 

Kila mara niligeuza macho yangu huku na kule nikiwa kwenye korido naelekea chumba cha  mwisho ambacho ndimo lile shimo la kuelekea kaburini lilikuwamo. Nilipofika niliuwona  Mlango ukiwa umefungwa, sauti ya kuimba wala haikukoma isipokua ilikua ikihama kadiri  nilivyokua najaribu kusogea hadi nilipofika Mlangoni. 

Kitasa cha mlango kilikua kinaniangalia Mimi, nami nilikitazama huku mkono wangu ukiwa na  shahuku ya kukitekenya kitasa hicho chenye rangi ya dhahabu, kitasa cha kizamani chenye  urembo wa maua. Niliutoa mkono wangu, ukasogea hadi kukikamata kitasa kisha nikakitekenya  kikatoa sauti ya kufunguka. 

Upenyo mdogo ulionekana baada ya mlango kufunguka kidogo, nilihitaji ujasiri wa ziada ili  kupeleka macho yangu ndani. Mwili ulianza kusisimka, nywele zilinisimama kichwani mwangu 

Haikua hali ya kawaida, ilikua ni hali ya hatari. Mara nilianza kusikia sauti ya kitu kikitembea,  kwa namna nilivyokua nakisikia kitu hicho wala hakikua Binadamu wala Mdudu isipokua ni kitu 

cha ajabu sana, kishindo kilikua kinasikika kwa uzito sana halafu paliongezeka sauti nyingine  kama ya kiatu kirefu cha kike hivi. Sauti hiyo ilikua ikisikika nyuma yangu, niligeuka haraka  kuangalia, niliambulia kuona kivuli cha kutisha sana. 

Kiumbe hicho kilikua bado hakijafika kwenye ile korido ya kuelekea chumbani, nilifikiria nini  cha Kufanya. Haraka Ubongo wangu ukaniambia niingie ndani ya chumba hicho maana nyuma  palikua haparudiki. Niliingia halafu kwa taratibu sana niliufunga mlango, nikawa nimejifungia,  sauti ya yule Mwanamke kuimba ilikoma. 

Pakawa kimya sana, ndani ya kile chumba cha stoo kilikua vile vile, vitu vingi tulivyoviweka  vilikaa kwa mpangilio ule wa Mwanzo, nilitafuta lile shimo la ajabu lakini halikuwemo. Sasa  nikaona ni bora nijifiche huwenda kile kiumbe cha ajabu kingeweza kuingia ndani ya kile  chumba. 

Nilijibanza mahali nikisikiliza nini kitakachotokea, ile sauti ya kishindo ilianza kuja karibu nami.  Nilizidi kuogopa, jasho la hofu lilikua likinimwagika 

Kile kishindo kiliishia mlangoni kisha palikua kimya sana. Kimya kiliendelea kwa kitambo  kirefu kama cha dakika kumi na tano hivi hadi nilianza kujiuliza maswali mengi yasiyo na  majibu. Kwanza nilijiulza kishindo kile kilikua cha kiumbe gani, pili nilijiuliza kiumbe hicho  kilikua kimeondoka pale mlangoni au nini kilimfanya awe kimya. 

Nikataka kujua, nikasimama ili nielekee mlangoni, mara ghafla mlango ulifunguliwa haraka  sana, pale pale nilijibanza tena kwa uhakika kabisa kua sijaonekana, ule mlango niliupa bega  huku shingo yangu nikiwa nimeikata upande mwingine. Sikutaka kuangalia ni Nani aliyeufungua  ule mlango 

“Celin upo hapa?” nilisikia sauti ya yule Bibi jini, nilizidi kutetemeka. Nikauziba mdomo wangu.  Aliendelea kuniita kwa sauti ya kunong’ona, sauti yake ilikua na nguvu sana kiasi kwamba  nilijizuia sana nisiitikie 

Sikujua kama alikua amegundua nipo ndani ya kile chumba au la. Niliendelea kupumua kwa shida, nilisali sala zote. Basi, naona hakuwa na uhakika kuwa nipo ndani ya kile chumba 

Taratibu nami nilitaka kumwona, nilikua na uhakika kwa asilimia zote kua hajagundua chochote.  Niligeuza shingo yangu taratibu huku macho yangu yakiwa makali niweze kumwona,  nilipofanikiwa kugeuza shingo ndipo nilipokiona kiumbe cha kutisha sana. 

Kwa uhakika alikua na umbo la Binadamu, alivalia gauni chakavu lenye rangi nyeupe, nywele  zake zilikua chafu pia halafu ni ndefu sana kiasi kwamba zilikua zinakaribia kiunoni mwake.  Alikua na kucha ndefu sana kama ndege tai, alikua amenipa mgongo na laiti kama  angelinionesha sura yake basi ingelikua mbaya zaidi. 

Miguuni alikua na kwato kama za ng’ombe, kiukweli kilikua kiumbe cha ajabu kuwahi kukiona  maishani mwangu. Mwili ulikua unaendelea kusisimka tu, cha ajabu baada ya dakika kama moja 

na ushee hivi alibadilika kutoka kwenye lile umbo na kua yule Bibi Kizee ambaye ni jini  Muuwaji 

Moyo wangu ulizidi kwenda mbioo nikikumbuka namna alivyosababisha nikamuuwa Mama  yangu, kifo cha Zena na Caren chanzo ni yeye. Aligeuka huku na kule kama vile alikua  akihakikisha kua hakuna anayemwona. Kisha alisogea mbele kidogo karibu na pembe ya ukuta  akasema 

“Fungukaa‼” sauti yake ilikua kali ya kutisha, mara lile shimo la ajabu lilifunguka. Huu sasa  ndio mlango wa kuelekea kaburini kwenye nafsi ya Sabra, shimo namna lilivyofunguka  lilinishtua sana nikakumbuka ile siku nilimwona Baba na Mama wakitoka kwenye shimo lile  wakiwa uchi wa mnyama. 

Nilimwona yule jini akiingia ndani ya shimo hilo lenye rangi jekundu, lilikua mfano wa mlango  wa Andaki hivi lenye kuwaka rangi nyekundu na moshi mithiri ya mvuke wa maji ya moto.  Baada ya yeye kuingia ndani ya shimo palijifunga kama vile hapajatokea kitu chochote 

Nilistaajabu sana, nilisogea taratibu kwa tahadhari kubwa. Hapakua na shimo lolote wala dalili  kwamba pana mlango, nililitafuta lakini ilikua ni sawa na kujiuliza maswali yasiyo na majibu.  Nilibaki nikiwa nimesimama sijui naanzia wapi ili nami niingie humo kwenye shimo labda  ningeweza kuipata mafsi ya Sabra. 

Roho iliniuma kuona nimefeli zoezi muhimu sana ambalo lilikua ni hatua kubwa kwangu kufikia  hitimisho ya matatizo yanayoikumba familia yangu. Nilifikiria nami nifanye kama alivyofanya  ili lile shimo lifunguke. Nilisogea pale karibu na pembe ya ukuta kisha nikasema 

“Funguka‼” mara ya kwanza hapakua na chochote kilichotokea, nikarudia tena na tena. Zaidi ya  mara tano lakini shimo halikutokea. Nilitamani nilie maana sikua na uwezo wa ziada wa  kutambua mambo mengi isipokua machache ambayo yule Mwanaume aliyejitambulisha kama  Haji aliniambia 

Basi nilikata tamaa, chozi lilinibubujika. Nikajikuta nikipandwa na hasira sana, nikasema kwa  mara ya mwisho kwa sauti kubwa ya hasira huku chozi likinibubujika 

“Fungukaaa‼!” ghafla tu nililiona lile shimo la ajabu likifunguka nyuma yangu, palikua panatoa  mvuke na joto kwa mbali, rangi nyekundu ilikua imelizunguka shimo lile, nilichungulia ndani ya  shimo maana sikuwahi kuingia hivyo nilikua sijui chochote kile hata kunaonekanaje nilikua sijui. 

Nilitumia muda mrefu nikiliangalia tu, kisha niliisikia sauti nzito ikiuliza kutoka ndani ya shimo.

Nini Kitaendelea? Usikose Sehemu Ya KUMI

COMMENTS ZIWE NYINGI SASA 

JIUNGE NA KIJIWENI WHATSAPP CHANNEL Kwa Kugusa Hapa 

Soma Riwaya Nyingine Za Kijiweni Kwa KUGUSA HAPA

Wewe kama MFANYABIASHARA.. Kuna wakati unatamani kuwafikia watu wengi zaidi na hujui wapi pa kuanzia , USIJALI kwani hapa ndipo ambapo MTAA UNAONGEA na tuko tayari kukusaidia kuwafikia watu wengi kwa BEI YA OFA

Njoo Utangaze Nasi Sasa Kwa Kutuambia Una TANGAZO Gani na unataka kutangaza kwa muda gani kwa kutuma ujumbe hapa WwhatsApp Kupitia Namba +255760871896 

Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx

 

 

10 Comments

Leave A Reply

Exit mobile version