Ndugu Mhariri leo naomba kuandika kuhusu jambo ambalo wengi hawalizungumzi haswa kuhusu beki wetu Inonga.
Nimefuatilia sana barua zako ambazo umekua ukizichapisha hapa Kijiweni na nimeona nishiriki kwa kuandika kuhusu jambo hili ambalo lipo ndani ya uongozi wa klabu yangu pendwa yenye mitaa yake ya Msimbazi.
Kumekua na taarifa mbalimbali kuhusu maamuzi magumu ambayo viongozi wanafikiria kuyafanya katika kuhakikisha kuwa kunakua na maboresho ndani ya klabu ya Simba haswa katika nafasi ya uongozi pamoja na katika kikosi chetu yaani nikiamaanisha wachezaji na niseme tu kuwa katika yale maamuzi magumu ambayo viongozi wanapaswa kuyafanya wakati huu bila kufikiria mara mbili mbili ni pamoja na kumuuza Henock Inonga.
Mhariri, sio kwamba namchukia beki huyu walaa ila tu ni kwa manufa yetu kwani nimemtazama katika mechi kadhaa ambazo amekua akicheza toka atoke katika michuano ya mataifa barani Afrika ambapo walishika nafasi ya 4.
Inonga wa sasa hivi akiwa uwanjani sio yule wa misimu miwili ya nyuma, huioni seriousness yake wala kujutia makosa yanayojirudia rudia. Kuna namna kama moyo wake haupo tena kuipambania Simba na ni kama anafikiria kuondoka klabuni.
Inawezekana yupo kimwili, lakini sio kiakili, hata uchezaji wake hajitumia kama zamani, mara nyingi anaonekana anatembea na hata hakabi kwa nguvu ile aliyokuja nayo Simba. Kwenye mitandao yake ya kijamii, Inonga ameweka emoji za kulia na kuaga huku akiandika ‘bye’ (kwa heri/kwa herini) bila kufafanua.
Kwa taswira hiyo hakuna nafasi ya kumshawishi kubaki bali kumfungulia milango atafute changamoto mpya. Klabu itapoteza beki mkubwa, lakini itaingiza pesa ndefu ya kutafuta Inonga mwingine wa daraja la juu. Wapo wengi sokoni.
Nakutakia majukumu mema na ahsante kwa kuisoma barua hii.
SOMA ZAIDI: Barua Kwako Mo Dewji Rais Wa Heshima Simba Sc



