Ilipoishia ” Dakika saba pekee zilitosha kwa Marcus kupata mahali pa kuanza Uchunguzi wake, walitolewa vijana hao wakiwa wamevimba sehemu mbalimbali za Miili yao.”
Tuendelee Sasa
SEHEMU YA KUMI
Wiki mbili baada kifo cha Mzee Yusuf.
Adela alikua ameketi chumbani kwake huku mkononi akiwa ameshikilia kadi moja, aliikumbuka kadi hiyo alipewa na Babu Yake Marehemu Bilionea Yusuf. Kadi ilikua na Namba na Jina lililoandikwa Susan Mbeno.
Aliitafakari kadi hiyo, Mungu aliweka akili ya kiutu uzima kwa Binti huyu wa Kitajiri. Kipawa cha kufikiri kilikua juu sana tofauti na umri wake, aliitazama kwa zaidi ya dakika sita huku akitafakari ni kwanini Babu yake alimpatia kadi hiyo, moyo ulimdunda.
Akaielekea simu ya Mezani na kuipiga namba hiyo akiamini Babu yake alihitaji yeye azungumze na huyo Susan Mbeno, akiwa anasubiria simu ipokelewe alikua akitetemeka huku akijawa na woga wa ajabu sana, kabla hata haijapokelewa aliikata.
Akaketi kitandani akiwa analia huku akisema
“Sitaki, sitaki, staki” sauti hii ilipenya kwenye masikio ya Bi Choro aliyekua akipiga deki sakafu kando ya chumba cha Adela, ikampeleka hadi chumbani humo na kumkuta akiwa analia.
“Adela unalia nini?” alihoji Bi Choro kwa upole sana
“Bibi sitaki kusema, sitaki Mimi” alisema Adela akimkumbatia Bi Choro
“Hutaki kusema nini?”
“Bibi sitaki Mimi” alisema akiwa analia, Bi Choro alijitahidi sana kumhoji Adela lakini hakusema kingine zaidi ya kudondosha chozi.
“Basi pumzika Adela, usiwe na hofu, usiogope. Mlinzi yupo, Mimi nipo hakuna mwingine
atakayekuja, upo salama sawa?” alisema Bi Choro, aliamini kifo cha Mzee Yusuf ndiyo sababu ya Binti huyo kulia kwani kipindi hicho alikua akisakamwa sana na wapelelezi.
Baadaye Adela akapitiwa na Usingizi, Bi Choro akamlaza vizuri kisha akatoka.
***
“Mapigo yake ya moyo yanazidi kushuka, jitihada zifanyike haraka” ilikua ni sauti ya Dokta
akiwaelekeza Madaktari na Manesi ambao walikua ndani ya chumba kimoja alicholazwa Adela,
mitambo ilionesha kushuka sana kwa mapigo yake hali iliyoonesha wazi kuwa angefariki muda
mchache Ujao. Alikua akishindwa kuhema, macho yalimtoka pima.
“Mwanangu Mimi, Adelaaaa” Sofia alikua akimlilia Binti yake, walikesha hapo kwa usiku mzima na nusu ya siku mpya, Hamza hakumwacha Dada yake.
Akamweleza kua Madaktari wanafanya jitihada ili kuokoa Maisha ya Binti huyo lakini hiyo haikutosha kumtuliza, alilia mfululizo.
Jioni saa 10:12 Daktari aliandika muda ambao Mtoto Adela alifariki Dunia, taarifa iliyomfanya Sofia apoteze fahamu zaidi ya mara tano. Kifo cha Binti huyo kiliandikwa na Daktari aliyekua akimtibia kua alifariki kwa mshituko wa moyo uliotokana na njozi aliyokua ameiyota Binti huyo, sisi tunaifahamu ndoto ya Binti huyo lakini taarifa ya kifo hicho kiliwashangaza walio wengi.
Maneno ya chini chini yakawa mengi, familia hiyo ikatajwa na walioifahamu kuwa inaandamwa na mzimu wa kifo, wengine wakihusisha vifo hivyo na imani za Freemason lakini kwa mpelelezi Daudi Mbaga aliyeko Kigoma aliuona urejeo wa Muuwaji ndani ya familia hiyo, saa 12:00 kengele ya Kanisa la Roma ilipokua ikigonga, Daudi Mbaga alimpigia tena simu Jasusi Marcus aliyekua kituo cha Polisi walipohifadhiwa wale Wanachuo.
“Nitazungumza nao baadae, warudishe Mahabusu” aliagiza Marcus huku simu ya Daudi Mbaga
ikiwa hewani, akakimbilia nje sehemu ambayo aliamini ni salama zaidi kuipokea
“Nasikiliza” alisema Marcus
“Binti Adela amefariki, mwili upo St. Augustino Hospital Kinondoni, wahi ukauchunguze Marcus”
Ilikua ni taarifa iliyomshtua Marcus, Adela alikua ni miongoni mwa Watu walio katika listi yake ya upelelezi ikiaminika kuwa ndiye aliyemuona Muuwaji kwa mujibu wa ripoti ya Daudi Mbaga.
“Yule Binti amefariki?”
“Ndiyo, nasikia kifo chake kimetokana na ndoto aliyoiota, hii haiwezekani Marcus, lipo jambo nyuma yake”
“Sawa, natoka hewani” alisema Marcus kisha alikata simu. Alichezesha kope za macho yake huku akiwa amejawa na Mshangao, watasemaje amefariki kutokana na ndoto tu? Hata yeye akatia walakini kua Muuwaji amerudi tena, hii ikaongeza joto zaidi la kuamini Sakina hakua Muuwaji halisi.
Saa moja mbele, Marcus anafika Hospitali Kinondoni alipoelekezwa na Daudi Mbaga. Hakuwapigia simu wafiwa, alifika na kuuliza Mapokezi, kwanza alijitambulisha kua ni Askari polisi kisha alisema
“Nimekuja kumtazama Mgonjwa anaitwa Adela kutoka katika familia ya Bilionea Yusuf” alisema, kwa heshima ya kazi yake, Binti aliye mapokezi akachota taarifa haraka kwenye kompyuta ili kujua kama walikua na Mgonjwa anayeitwa Adela kutokea kwenye familia ya kitajiri.
“Samahani, ameshafariki”
“Mwili wake uko wapi?”
“Mochwari daraja la kwanza”
“Ahsante” akasema Jasusi Marcus, Yule Mdada akamuelekeza mahali ilipo Mochwari daraja la
kwanza ambalo Miili ya watu matajiri iliwekwa huko tena ilikua michache mno. Akaishika korido aliyoelekezwa, akiwa amebakisha hatua kadhaa kufika alipishana na Daktari Mmoja, akamsimamisha.
Lengo la Marcus lilikua ni kumsalimia kisha amuulize kama Mochwari kuna waangalizi wa maiti, Daktari huyo alionekana kuwa mwenye hofu sana, mkononi alikua na Bahasha ya kaki iliyotuna.
“Samahani, Naitwa Marcus ni afisa wa polisi. Nauliza kama muda huu kuna waangalizi wa maiti” alisema Marcus, yule Daktari wa kiume akawa anababaika kumjibu Marcus akionekana kujawa na woga fulani ndani yake hadi Marcus alishangaa, mara ile bahasha ilianguka na bunda moja la pesa likatoka, haraka yule Daktari akaliokota na kulirudisha kwenye Bahasha akioneka kuwa na hofu sana kisha akaondoka bila kumpa jibu la Uhakika.
“Daktari anapata wapi bunda la pesa tena akiwa sehemu ya kazi?” alijiuliza Marcus kabla ya
kupuuzia, mawazo na akili yake yakawa kuelekea Mochwari.
Akafika mbele ya Mlango wa Mochwari, aliona mlango ulikua na upenyo fulani wa wazi ambao
ulionesha ndani, ilionekana aliyeingia au kutoka aliacha Mlango wazi, wakati analitafakari hilo
alimwona Mtu aliyefunika sura kwa kutumia kofia ya koti jeusi akiwa ana randa randa Mochwari
tena hakuonekana kabisa kuwa Daktari.
Mavazi pekee yalimfanya Marcus achomoe Bastola yake kisha taratibu akaufungua mlango huo
ambao ulionekana kumpa taarifa Mtu aliye ndani ya chumba hicho, naye akaganda huku akiwa
ameshikilia jokofu moja la kuhifadhia Maiti.
“Wewe ni Nani?” aliuliza Marcus, lakini Mtu huyo alionesha wazi kua ni Mwoga. Alikua akitetemeka, alikua amempa mgongo Marcus aliye mita kadhaa.
“Nakuuliza tena, wewe ni Nani?” akahoji Marcus huku akiwa amenyoosha vizuri Bastola yake, kama alivyoambiwa na Daudi Mbaga naye hisia zake akazihamishia hivyo hivyo kua kifo cha Mtoto Adela si kifo cha Mshituko kama ambavyo ripoti ya Daktari ilisema, alihisi uwepo wa mambo yasiyo ya kawaida.
“Geuka taratibu mikono ikiwa juu” akapaza sauti Marcus huku akiamini moja kwa moja kua huyo Mtu si Mzuri ndiyo maana alikua akipekua kwenye Majokofu hayo. Mtu huyo akageuka huku kichwa akiwa amekiinamishia chini, Marcus akamtaka ainue kichwa chake.
Taratibu akainua kichwa akiwa anatetemeka, Marcus hakuyaamini macho yake. Mtu huyo alikua nani? ZIKIFIKA COMMENTS 100 naahia sehemu ya 11
Jiunge WhatsApp Channel Ya KIJIWENI Ili Kuwa Wa Kwanza Kupata Updates Za RIWAYA Hii Kwa Kubonyeza Hapa
SOMA Uchambuzi Na Makala Mbalimbali Kwa Kubonyeza Hapa



