Ilipoishia sehemu ya tatu ya In the name of LOVE

“Basi hakuna shida Zaylisa, mnaweza kuishi wote ikiwa jambo lako la  talaka litakamilika” maneno ya Clara yalinipa tabasamu kubwa, basi  Tuliachana na Zaylisa ambaye aliaga kua anarudi kwake. 

Mimi na Clara tuliondoka Kisha tulimpitia Mtoto wake ambaye ni Melisa,  Kisha tulielekea nyumbani kwa Clara. Kila kitu kilikua kipya kwangu,  niliyaona mazingira yakiwa mageni kabisa, sikukumbuka kuhusu Mtoto  Melisa kua ni Mwanangu wa Damu kabisa na Clara ni Mke halali wa ndoa.  Endelea

SEHEMU YA TANO

Tulipofika, nililishangaa jumba Zuri sana la kifahari. Tulifunguliwa geti na  kuingia ndani, mahali ambapo niliishi kwa Miaka mitano sikupakumbuka  tena. Msichana wa kazi alitupokea na kunipa sura ya Ugeni kama alikua  akiniona kwa mara ya kwanza 

“Hapa ndio nyumbani kwangu Jacob, jisikie huru kabisa” alinikaribisha 

“Asante sana Clara, nitajisikia hivyo taratibu” Mara zote Melisa alikua  akinitazama sana kama Alikua akitaka kuniambia kua Mimi ni Baba yake  lakini aliishia kuwa mnyonge tu, Kuna kitu Cha ajabu ambacho  nilikishangaa sana. Mara zote nimwonapo Melisa nilihisi Upendo mwingi  sana juu yake. 

Nilioneshwa chumba changu Cha kulala, baada ya kuingia chumbani basi  Mtu pekee niliyemfikiria alikua ni Melisa mdogo wangu lakini niliamini  pengo lake lingezibwa na Zaylisa. 

Ndani ya chumba hicho palikua na picha ya Melisa akiwa na Mama yake,  hapakua na kumbukumbu nyingine. Niliketi pembeni ya Kitanda, Kila  nilichokigusa kilinianbia kua ilikua ni mara ya kwanza naingia hapo lakini  nafsi yangu ilianza kupata wasiwasi kua kama niliwahi kua hapo, iliponijia  hisia hii nilianza kuhisi maumivu makali ya kichwa. 

Nilihisi kama naishiwa nguvu nikajikuta nikijiinamia, mara Mlango  uligongwa. Sauti ya Clara ilipenya Ngoma za masikio yangu, nilijikuta  nikimkaribisha huku nikiwa ninajisikia vibaya. 

Alipoingia ndani, alinikuta nimejiinamia. Akajaribu kunikagua  nikamwambia anipe dawa zangu. Haraka alipekua Begi na kutoa dawa,  akanipa nikameza Kisha akaketi huku akifuatilia Hali yangu 

“Jacob, unajisikiaje?” aliniuliza, niligeuka kumtazama.  

“Nilihisi kama Kuna kitu kilikua kinakuja kichwani kwangu lakini kiligoma,  sijui ni kitu gani Clara” alinitazama kabla ya kunijibu.

“Bado Hali Yako haijatengemaa Jacob, unahitaji muda zaidi wa kupumzika.  Basi, ngoja nikuletee chakula” alisema akanyanyuka, nikamshika mkono.  Namna nilivyomshika nilihisi Kuna uhusiano Fulani kati yetu, lakini ni  uhusiano gani usiojitokeza, sikuweza kuelewa. Ghafla nilimwacha 

“Nahitaji kupumzika kwanza Clara, nitakula nikiamka”  

“Basi sawa. Pumzika Jacob, nitakuona baadaye” alisema Kisha alifungua  mlango na kuondoka, aliniachia maswali mazito sana. Akili yangu  iliniambia kua sikuwahi kua na rafiki kama yeye lakini nafsi iliniambia  palikua na uhusiano uliojificha, sikutaka kuumiza akili yangu.  

Nilipanda kitandani pole pole, punde Usingizi ulianza kuninyemelea  nikajikuta nikilala. 

** 

Siku iliyofuata, niliamshwa na sauti ya kugongwa kwa mlango. Nilijiinua  pole pole bila kusema chochote, nilitembea kwa kupepesuka kidogo  kutokana na usingizi Hadi mlangoni. Nilipofungua nilikutana na Clara 

“Habari ya Asubuhi Jacob” alinisalimia, namna alivyokua akinijali  ilinishangaza sana. 

“Nzuri sijui wewe na Melisa wako” 

“ Sote ni wazima Jacob. Nimekuandalia chai, jitahidi ukapate kifuangua  kinywa” 

“Sawa” Niliitikia, lakini nilikumbuka kuhusu Zaylisa 

“Hakupiga simu?” 

“Nani?” 

“Zaylisa” 

“Bado, Jacob kwasasa angalia zaidi afya Yako. Zaylisa atakuja usiwe na  wasiwasi sawa?” alisema huku akitabasamu kama vile alikua akiongea na  Mtoto mdogo. 

“Clara, baada ya Mdogo wangu Melisa anafuatia Zaylisa. Sijawahi  kumpenda Mwanamke mwingine zaidi yake, uwepo wake ni tiba kwangu”  nilisema kwa utulivu sana, nilikua usoni kwa Clara, alionekana kukosa  Raha kama Mtu anayekaribia kulia muda wowote 

“Kwanini nimtajapo Zaylisa wewe unakua hauna amani Clara? Nakupa  mzigo mzito Mimi kuishi hapa?” 

“Hapana Jacob, nimeona ni jinsi gani uliamua kupenda kwa moyo wako  wote. Hakika Zaylisa hawezi kukusahau kamwe” Nilitabasamu, maneno  yake yalikua kama kisu kwenye mfupa. Yaliingia Hadi ndani kabisa ya moyo  Wangu na kunipa Raha sana 

“Clara, ninapopenda nazama mazima. Najua kupenda sana Ndiyo maana  nilipomchagua Zaylisa sikuwahi kujutia” nilisema, hakuonekana kua na  Raha kabisa 

“Basi twende tukapate kifuangua kinywa Jacob” alisema, Taratibu Hadi  tulipofika Mezani, Melisa alikua hapo akinitazama sana kama kawaida  yake. Nami nilimwachia tabasamu 

“Baba” aliita Melisa, niligeuka kuangalia nyuma yangu pengine kulikua na  Mwanaume mwingine, niligundua hapakua na mwingine. Macho ya Melisa  yalikua yakinitazama Mimi tu huku akiwa analengwa na Mchozi  

Sikutegemea kama angeniita Baba, kwangu alikua Mtoto mgeni, lakini  kwake nilikua muhimu lakini kwenye kumbukumbu nilizozisahau,  nilimtazama Clara ili kupata taswira ya alichokisema. Niliona alikua  akionekana ni mwenye huzuni ya ndani kama Mtu anayevuja damu ndani  kwa ndani. 

Sikujua Baba yake Melisa alikua wapi, hatukuwahi kuzungumzia Hilo Mimi  na Clara. Nilihisi labda Melisa alikua amemkumbuka Baba yake, basi  nilitabasamu tu Kisha nikamwambia 

“Unasemaje Binti yangu?” nilihisi kama ninaongea na Mtu ninaye fahamu  vizuri lakini nisiyemkumbuka. Melisa alimwangalia Mama yake. Kisha  alinyanyuka na kuondoka pale akaelekea chumbani, Clara akaniambia 

“Samahani ngoja niongee na Melisa” Kisha naye aliondoka hapo, Kuna  namna nilianza kujihisi. Ni kama Nina mzigo Fulani ndani yangu. Mzigo  ambao ulikua ukinielemea Kila nilivyomwona Melisa.  

“Au kwasababu ana jina la Marehemu mdogo wangu?” nilijiuliza. Kabla  hata sijazama sana kifikra, mara Mlango uligongwa. Dada wa kazi hakua  karibu, niliona ni Bora nielekee mlangoni. 

Taratibu sana nilisogea, nilipofungua mlango nilimwona Zaylisa. Alikua  amesimama akinitazama kwa tabasamu sana, niliishiwa hata neno la  kumwambia. Nilimkumbatia kwa hisia kubwa sana, moyo Wangu  uliniambia kua nilikua namkosa ndani yangu

Tukiwa hapo, nyuma yangu alikuja Clara. Alisimama akitutazama,  nilipoacha kumkumbatia Zaylisa niligeuka, niliuwona Mshangao mkubwa  ambao Clara alikua nao, nilipomtazama Zaylisa niliona sura ya tofauti. 

Alikua akimtazama huku kama alikua akimtumia Clara ujumbe wa hisia  ambao sikuweza kuelewa kabisa. 

Macho ya Clara yaliingiwa na huzuni, kidogo chozi lilikua likimlenga lakini  Zaylisa alikua na sura kavu.  

“Clara” alisema Zaylisa, alionesha pia sura ya Huzuni, akamfuata Clara  alipokua amesimama Kisha akamwambia 

“Samahani, najali kuhusu Hali ya Jacob. Nitakua hapa kwa ajili yake” Clara  akamtazama sana Zaylisa 

“Hatukukubaliana hili si Ndiyo? Sasa unafanya nini?” alisema kwa sauti ya  chini lakini niliweza kusikia, Kisha Zaylisa akageuka na kunitazama. 

“Babe! Nitakua hapa kwa ajili Yako” nilitabasamu lakini nilikua na maswali  mengi kichwani, Zaylisa ni Mke wa Mtu angewezaje kukaa na Mimi? 

“Lakini wewe si?…” kabla hata sijamaliza kuongea alinikatisha akasema 

“Ndiyo, lakini sasa siyo Mke wa Mtu tena. Talaka hii hapa” alisema  akaonesha bahasha aliyokua ameishikilia mkononi, Mimi na Clara  tulitazamana kwa Mshangao. Japo nilikua nahitaji sana kua na Zaylisa  lakini alichosema kilinishtua kidogo.  

Niliipokea bahasha, nikaifungua pole pole. Ndani yake mlikua na karatasi  tatu zenye maandishi ya kuchapwa. Palindikwa ‘TALAKA’ 

Moyo ulinienda mbio, palikua na Saini zao kua walikua wameachana.  Sikujua nifanye nini kati ya kufurahi au kuendelea kuuliza, hata hivyo  ningeuliza nini tena wakati tayari Kila kitu kipo kwa maandishi, lakini uso  wa Clara ulijawa na Mshangao na huzuni iliyochanganika na hasira. 

Nilihisi furaha Iliyo changanika na hisia ya maumivu, sikua na  kumbukumbu ya kumpenda Mwanamke mwingine isipokua yeye. Nilijikuta  nikimkumbatia kwa nguvu Zaylisa mbele ya Clara 

Clara hakutaka kututazama, aligeuka pembeni akiwa analia Kisha alifungua  mlango akaingia chumbani kwake.  

“Kwanini Clara anaonekana ana huzuni kukuona wewe?” nilimuuliza  Zaylisa, alinitazama akitabasamu kidogo huku akionesha vishimo kwenye 

mashavu yake. Akanishika mabegani kwa mahaba mazito sana, akaniambia  huku akinitazama usoni kama vile ilikua ni mara ya kwanza tunaonana 

“Jacob, siwezi kujua labda hakutaka niwe hapa” alisema, nilishusha pumzi  kidogo. Clara ni Mtu wa muhimu sana aliyenisaidia nilipopata ajali hivyo  kubadilika kwake kulinipa maswali mengi yasiyo na Majibu.  

“Najisikia huzuni sana, siiyoni Nuru machoni pake. Nahisi Kuna kitu  hakipo sawa kwake”  

“Hata hivyo karibu, nitaongea naye…” nilisema Kisha nilikamata Begi lake,  akanishika mkono akaniambia 

“Jacob, usimuulize chochote kile. Mimi nitaongea naye, sawa?”  niliyatazama macho ya Zaylisa, yalikua ni macho Yale Yale yaliyojawa na  Upendo ule ule, sikua na shaka naye. Nilitabasamu kidogo 

“Sawa babe” nilikokota Begi, nikamshika mkono Zaylisa Kisha nikaelekea  naye chumbani kwangu. 

Tulipofika chumbani ni kama tuliamsha mashetani ya mapenzi, japo Bado  nilikua sijapona vizuri lakini sikutaka Usiku unipite, nilikula tunda lililokua  limekaribia kuchukuliwa na mwingine. Lakini Kila sekunde nilihisi palikua  na Mtu mlangoni, ile amani ilianza kuondoka 

“Vipi?” aliniuliza Zaylisa akiwa anajilaza kando baada ya kuona kama akili  yangu haipo. 

“Hakuna” nilitabasamu ili kumwondoa hofu lakini haikumsaidia akaniuliza “Unahisi afya Yako inabadilika?”  

“Hapana, unajua baada ya ajali Kuna vitu vipo kichwani ila sijui ni nini,  Wacha nipate Maji ya kunywa kidogo” nilisema Kisha nilivalia pensi,  nikamwacha Zaylisa Kitandani, nikafungua mlango nikaelekea sebleni. 

Nilishangaa kuona taa ilikua Bado inawaka na hapakua na dalili ya uwepo  wa Mtu, basi nikaona nipate Maji kwanza Kisha nizime. Nilipofika kwenye  friji nilihisi Hali isiyo ya kawaida, kama vile palikua na kumbukumbu  Fulani ya Mimi kufika hapo kabla lakini sikutaka kuipa nguvu sana  kumbukumbu hiyo, nilihisi ni wenge tu. 

Upepo ulivuma kidogo ukapeperusha pazia, nikamwona Clara akiwa  amesimama varandani kwa nje, alikua kama analia hivi. Niliacha zoezi la  kuchukua Maji, nilimtazama kwa makini sana akiwa anaangalia pembeni  bila kujua nilikua nikimtazama.

Upepo ulikua ukisukuma nywele zake, nilipata shahuku ya kutaka kuongea  naye. Nilielekea mlangoni nikafungua mlango taratibu, sauti ya mlango  ilimfanya ashtuke na kugeuka. Aliniona nikiwa nimesimama mlangoni  nikimtazama, alikua akidondosha chozi bila kuficha. 

Tulitazamana bila kusemeshana kwa sekunde kadhaa huku nikitafakari  nini maana ya chozi lake, mbona Kila niwapo karibu naye hua nahisi Hali  isiyo ya kawaida. Nilisogea taratibu nikimtazama, macho yetu yalikua  thabiti yasiyo kwepana  

Hadi namfikia hakuna aliyeongea na mwenzake, nilijikuta nikimweka vizuri  nywele zake.  

Nini Kitaendelea? Usikose sehemu ya TANO

JIUNGE NA KIJIWENI WHATSAPP CHANNEL Kwa Kugusa Hapa 

Soma Riwaya Nyingine Za Kijiweni Kwa KUGUSA HAPA

Wewe kama MFANYABIASHARA.. Kuna wakati unatamani kuwafikia watu wengi zaidi na hujui wapi pa kuanzia , USIJALI kwani hapa ndipo ambapo MTAA UNAONGEA na tuko tayari kukusaidia kuwafikia watu wengi kwa BEI YA OFA

Njoo Utangaze Nasi Sasa Kwa Kutuambia Una TANGAZO Gani na unataka kutangaza kwa muda gani kwa kutuma ujumbe hapa WwhatsApp Kupitia Namba +255760871896 

Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love xx Love 

 

Leave A Reply

Exit mobile version