Ilipoishia Sehemu Ya Pili

“Kazi imeisha!” Alisema Diana kwa njia ya simu 

“Waoo Good Girl ( Vizuri Msichana mzuri ) ” ilisikika sauti  nzito ya kizee 

“Rudi Tanzania” Alimalizia kusema Mwanaume huyo kwa njia ya  simu, simu hiyo ilikatika, tayali polisi walishafika nje ya  Hoteli hiyo, Diana alichofanya ni kuingia kwenye chemba ya  maji machafu akaenda kutokea mbali na eneo hilo.  Endelea  

SEHEMU YA TATU 

Tayali ilifahamika ni wapi ambapo Faudhia angepatikana ni  mpaka wa Namanga, ilihitaji auawe kabla hajafika Tanzania. 

Mishale ya saa 11 Alfajiri vijana wa Khalid Bangala  walijaribu kumtafuta Bosi wao bila mafanikio, hawakujuwa  wafanye nini sababu maelekezo yote walikuwa wakipewa na Bosi  wao ambaye alikuwa ameshauawa Hotelini, majadiliano yao  yalimuamsha Faudhia akiwa ndani ya Sanduku. 

“Unafikiri tutafanya nini, Simu ya Khalid haipatikani,  tufanyaje na tunakaribia eneo lenye askari” Alisema mmoja wa  Vijana hao, Faudhia aliposikia hivi alihisi kuna hatari,  kutokana na mafunzo aliyoyapitia aligundua pengine kuna jambo  halipo sawa, aligonga afunguliwe huku akisema amebanwa sana  na Haja. Vijana hao walisimamisha gari hilo, walikuwa juu ya  mlima, kulikuwa kunapambazuka na iliwahitaji kutembea chini  ya Kilometa 15 kufika Mpakani. Faudhia hakutaka kujionesha  kuwa amehisi jambo lisilo la kawaida, hakutaka kuwaamini moja  kwa moja, walikuwa na bunduki ambazo walizificha, mmoja  alimsindikiza Faudhia kujisaidia huku akiwa amemshikilia  Bunduki kwasababu alikuwa bado hajawalipa 

“Pale ni wapi?” Alihoji Faudhia akiwa anazidi kusogea sehemu  ya kujisaidia 

“Longido” alijibu Mwanaume huyo 

“Unamaanisha Tanzania?” 

“Ndio, unapaswa kutulipa kwanza sababu umeshafika eneo husika  ambalo sisi hatuwezi kusogea huko, kuna ulinzi wa Askari wa  mpakani.” Alisema Mwanume huyo

“Simama hapo basi au unataka kunichungulia!” Aliuliza Faudhia  na kumfanya Mwanaume huyo asimame lakini akiwa anamuonesha  Bunduki Faudhia ambaye alikuwa tayali ameashaanza kujisaidia. 

Akiwa anajisaidia alisikia milio ya Risasi za haraka kisha  ukimya ulitanda, yule aliyemsindikiza alirudi kule haraka  akakuta wenzake tayari wameuawa, lilikuwepo kundi la watu  tano ambalo lilitokea msituni na kumtaka Mwanaume huyo  anyanyue mikono yake juu. Wanaume hao walikuwa wakiongea  rafudhi ya Kenya, haraka Faudhia alifungua kibegi chake  kidogo akatoa bastola yake, ukimya ulitawala, Faudhia  alijaribu kuchungulia eneo la tukio ndipo alipowaona Wanaume  hao, haraka alizama kwenye kichaka 

“Msichana yupo wapi?” Alihoji mmoja wa Watu hao huku akiwa  amenyooshea bastola yule kijana wa Khalid aliyebakia, yule  Mwanaume hakuwa na chaguo ilibidi aoneshe mahali ambapo  Faudhia alikuwa ameingia kwa ajili ya kujisaidia, alipigwa  risasi yule Mwanaume kisha lile kundi liliongoza mahali  ambapo Faudhia alikuwa ameingia, ilikuwa inakaribia saa 12  asubuhi, kulishaanza kupambazuka. 

Faudhia alishajuwa hali ya hatari ilikuwa imenukia eneo hilo,  alichofanya ni kuanza kukimbia kuelekea mpaka wa Namanga  upande wa kaskazini ambako ndipo ilipo Wilaya ya Longido,  alikuwa na maelekezo maalum ya eneo gani anapaswa kupita  ambalo litakuwa salama lakini kutokana na milio ya Risasi  kusikika iliwashtua askari wa mpakani wakatoka kwa ajili ya  kuangalia kulikuwa na tatizo gani. 

“Yule pale” Alisema kiongozi wa kundi hilo la Watu watano,  walipewa amri ya kumuuwa Faudhia kutoka kwa Mtu ambaye  hakujulikana hadi kufikia wakati huo, ila Faudhia alijuwa ni  kwanini Watu hao walikuwa wakimfuatilia ila hakujua wametumwa  na nani. 

Milio ya Risasi iliendelea kurindima msituni hapo, Faudhia  alijitahidi kukimbia ili kuokoa Maisha yake. Ulikuwa ni  mtafutano wa zaidi ya dakika 10 bila mafanikio kwa Wanaume wa  kundi hilo kumpata Faudhia ambaye alishahitimu mafunzo ya  ujasusi huko Mexico, Faudhia alifuata maelekezo maalum ili  aonane na Mtu mwenye gari msituni hapo, bahati mbaya akiwa  anakaribia alikutana na Askari wa mpakani ambao walikuwa  wakifuatilia milio ya Risasi, Faudhia alisimama kwa sekunde  kadhaa huku akiwa anatazama na Askari hao ambao walikuwa  mbele yake Mita kadhaa tuu kutokea aliposimama, pumzi za  Faudhia zilimwambia kuwa hatuna jinsi bali kufa au  kujikamatisha mikononi mwa Askari hao.

“Weka silaha yako chini” Alisema mmoja wa Askari hao, Kila  hesabu aliyokuwa anaipiga Faudhia haikumpa jibu linalotakiwa,  alijikuta akijisalimisha mwenyewe, Askari walianza kusogea  taratibu kwa makini sana eneo ambalo Faudhia alikuwa  amesimama, wale wanaume wa kundi la Kigaidi hawakujua kuwa  Faudhia alikuwa amesimama mbele ya kundi la Askari polisi,  walitokea eneo hilo na kushtukizwa na askari polisi kisha  mashambulizi ya Risasi yalianza kusikika huku haraka Faudhia  akichumpa na kujitupa kwenye poromoko dogo, Milio ya Risasi  iliendelea kusikika lakini haikufamfanya Faudhia asimame wala  arudi nyuma, alizidi kusonga mbele hadi alipofika mpaka wa  Namanga, alivuka na kuingia Tanzania. 

Mashambulizi baina ya Askari polisi wa mpakani na Lile kundi  yaliendelea na kumpa uhuru Faudhia kukutana na Mtu  aliyepangiwa kukutana naye mpakani hapo 

“Ingia kwenye gari haraka tuondoke eneo hili” alisema  Mwanaume mmoja ambaye ndiye aliyetakiwa kumchukua Faudhia  mpakani na kumfikisha Arusha Mjini, Faudhia aliingia ndani ya  gari na safari ilianza kuelekea Arusha Mjini. 

••••••••••••••••••••••••••••••••• 

Jeshi la polisi liliizunguka Benki kuu ( B.O.T ) ili  kuhakikisha hakuna anayetoka humo benki, ndani ya Benki hiyo  alikuwepo Mtu hatari aliyeitwa Chogo, tayari alikuwa amemteka  Mke wa Gavana na Gavana mwenyewe ambao wote walikutwa ndani  ya Benki hiyo, nje ya Benki zilionekana maiti za Askari  kadhaa ambao walikuwa wakitaka kufanya jaribio la  kushambuliana na Magaidi hao ambao walionekana kuzungumza  kiswahili kizuri, ilikuwa ni mishale ya saa 1 asubuhi jua  lilikuwa likichomoza, ukimya uliendelea kutawala na hakukuwa  na Raia aliyekuwa akifanya safari. Muda huo huo Mzee Shayo  aliwasili akiwa na gari yake, alikutana na Mkuu wa operesheni  hiyo aliyeitwa Sir Jeff, waliitana chemba kwa ajili ya  mazungumzo, wote walionekana kuanza kukata tamaa kwa jinsi  Magaidi hao walivyokuwa na mbinu kali za kukabiliana na  Askari. 

“Niambie mpango unaendaje?” Aliuliza Mzee Shayo huku  akitazama saa yake 

“Gavana na Mke wake wameshikiliwa ndani ya Benki” alijibu Sir  Jeff akiwa anamtazama Mzee Shayo 

“Hawajasema wanataka nini?” Aliuliza tena Mzee Shayo

“Hakuna hata mmoja aliyezungumza hadi hivi sasa zaidi ya  ishara tu kupitia kioo kikubwa” 

“Shenzi sana!!” alisema Mzee Shayo, punde simu yake iliita,  alipoangalia aliona ni Faudhia alikuwa akimpigia kwa njia ya  Whatssap, alisogea pembeni kuipokea sababu hakutaka  kunshirikisha yeyote juu ya Ujio wa Faudhia 

“Baba!! Nipo Arusha” Alisema Faudhia, hivi ndivyo ambavyo  Faudhia alikuwa akimchukulia Mzee Shayo, alimchukulia kama  Baba yake mzazi baada ya kumsaidia kumtoa kwenye mikono  hatari ya Mzee Shomari miaka mingi iliyopita 

“Sawa Faudhia! Nakutumia picha, nataka uchunguze huyo Mtu  anafahamika vipi hapo Arusha, ndiye mshukiwa namba Moja wa  tukio hili la Ugaidi” Alisema Mzee Shayo kisha alimtumia  picha Faudhia, ilikuwa ni picha ya Martin Gimbo ambaye  alijitambulisha kwa askari kama Chogo. Mara moja Faudhia  alianza kazi ndani ya Jiji la Arusha. Mfumo wa serikali  ulishawekwa kwenye kiganja cha Faudhia, alitumia kompyuta  mpakato ambayo alitumiwa na Mzee Shayo kupitia jamaa  aliyemchukua pale Mpakani, kompyuta hiyo ilikuwa na  mawasiliano na Kitengo cha Usalama wa Taifa, muda huo Faudhia  alikuwa Hotelini akiifanya kazi hiyo 

Aliingiza picha kwenye mtandao wa Idara ya Usalama wa Taifa,  alimuona jamaa huyo aliyeitwa Martin Gimbo. Taarifa za Jamaa  huyo zilionesha kuwa alizaliwa Arusha Mjini, aliona ni wapi  alisoma hivyo ilikuwa ni kazi rahisi kwa Faudhia, jua  lilikuwa limeshaweka makazi katika anga kwa ajili ya  kuimulika Dunia, Faudhia aliutumia usafiri wa gari waliyotoka  nayo mpakani akiwa na jamaa aliyeitwa Mohd, walienda kwenye  shule ambayo waliona kuwa Martin Gimbo alisoma, bahati nzuri  ilikuwa ni siku ya Shule, waliingia hadi ofisi ya Mwalimu  Mkuu, walienda shule ya Sekondari ambapo waliamini taarifa za  Martin zingepatikana. 

Walikaribishwa na Mwalimu mkuu wa shule hiyo ambaye muda  mchache baadaye aliketi kuwasikiliza huku akionekana  kuzishangaa sura za akina Faudhia 

“Naitwa Undercover Mohd kutoka kitengo cha Usalama wa Taifa”  alijitambulisha yule jamaa huku Faudhia akiwa kimya, Mohd  alitoa kitambulisho ili kumuaminisha Mwalimu huyo ambaye  alikuwa akitetemeka kutokana na woga sababu taarifa za ugaidi  zilizizima katika Miji mikuu ya Dodoma na Dar-es-salaam.  Baada ya kujiridhisha Mwalimu huyo alishusha pumzi zake kisha  aliondoa mawani

“Haikuwa rahisi kuwaamini sababu Wanafunzi na Waalimu  wameanza kukimbia Mji huu kwasababu ya uvumi kuwa baada ya  Dodoma na Dar utafuata Mji huu kuwa chini ya Magaidi” alisema  Mwalimu huyo kisha alishushia maji yaliyo ndani ya chupa,  alionekana kuwa na mengi ya kusema, alinyanyuka na kwenda  kufunga mlango kisha ndani kukawa giza aliwasha taa 

“Niwasaidie nini vijana?” Aliuliza Mwalimu huyo ambaye  alikuwa na mvi kiasi kuashiria kuwa umri wake ulikuwa  umeenda. Faudhia alitoa picha ya Chogo akamuonesha Mwalimu  huyo, Mwalimu aliichukua picha hiyo kisha aliisogeza kwenye  Mwanga, alishtuka baada ya kumuona chogo kisha alimpatia  picha Faudhia 

“Unamfahamu huyo Mtu?” Alihoji Mohd 

“Hapana” Alijibu Mwalimu baada ya kukaa kimya kwa sekunde  kadhaa 

“Mwalimu, ukweli wako utaliweka Taifa hili huru. Sura yako  inaonesha unamfahamu, tuambie anaishi wapi na unamfahamu  vipi?” Alidakia Faudhia 

“Nimesema simjui mnanilazimisha ili iweje? Simjui huyo Mtu  hebu nendeni” alisema Mwalimu kwa hasira huku akifoka mithiri  ya chatu aliyejeruhiwa 

“Unamjuwa huyu Mtu ndio maana unajaribu kuficha, Mwalimu  tuambie huyu Mtu anaishi wapi na unamfahamu vipi?” Alisema  Mohd kwa sauti iliyokauka 

“Nimesema simjui, hebu ondokeni ofisini kwangu haraka sana”  Alisema Mwalimu kwa sauti ile ile huku akinyanyuka kitini  mfano wa Mtu aliyetaka kuondoka ofisini hapo, Faudhia  alichomoa bastola na kumuonesha Mwalimu huyo. 

Bastola ilimfanya Mwalimu anywee kidogo 

“Endapo utaendelea kukanusha nitapasua ubongo wako sasa hivi,  unamjuwa huyu Mtu anaitwa Martin Gimbo. Alisoma hapa kwa  miaka minne” Alisema Faudhia akiwa amemshikilia Bastola  Mwalimu, 

“Sisi siyo Watu wabaya ila unatulazimisha kufanya huo ubaya,  kama hutaki kusema hebu tupatie faili la Martin” Alisema Mohd 

Mwalimu hakuwa na neno jasho lilikuwa likimtiririka, alivuta  droo la meza alitoa faili lenye maelezo yanayomuhusu Martin  Gimbo, Faudhia alipolifunua Faili hilo, halikuwa na picha ya 

Martin, halikuwa na maelezo kuwa Martin alikuwa akiishi  sehemu gani 

“Taarifa zimeenda wapi?” Alihoji Faudhia 

“Msijaribu kulifuatilia hilo jambo, hamtafanikiwa nawaambia,  mtakufa kabla ya kujuwa chochote kile” Alisema Mwalimu huyo 

“Ona hii” Alisema Mohd baada ya kuangalia kwa makini waliona  namba ya simu nyuma ya faili hilo, ilibidi walichukue faili  hilo, Mohd alichukua bastola na kumpiga mwalimu huyo. 

“Kwanini unauwa?” Alihoji Faudhia 

“Hana faida yoyote” Alisema Mohd 

“Tuondoke haraka sana” Aliongeza Mohd kisha waliingia ndani  ya gari na kutoweka eneo hilo, wakiwa ndani ya gari waliipiga  namba hiyo, ilipokelewa na Mwanamke mwenye sauti dhaifu sana,  ilionekana alikuwa mgonjwa maana alikuwa akikohoa sana 

Faudhia aliutumia ujanja wa mafunzo yake, walielekezwa alipo  mpokeaji wa simu hiyo, walienda kuonana naye lakini njiani  Faudhia alijiuliza Kwanini Mohd alimuuwa Mwalimu Mkuu baada  ya kuyatamka maneno yale? Hakutaka kuyapa kipaumbele,  walisogea hadi eneo husika, walikutana na Mama mmoja dhaifu  sana wa mwili wake, alikuwa akiishi na Mjukuu wake wa miaka  16 

Walimsalimia Mama huyo kisha walimuuliza 

“Hapa ni nyumbani kwa Martin Gimbo?” Alipouliza hivi huyo  Mama alipata nguvu hata ya kukaa, Mjukuu wake alishangaa sana  kwa Mama huyo kuketi mwenyewe wakati mara zote alikuwa  akimsaidia kukaa, Mama huyo alikaa kimya sana 

“Je? Wewe ni Mama yake Martin?” Alihoji Faudhia, Mama huyo  aliwatazama kisha aliwauliza 

“Mnamuulizia Martin Gimbo?” Aliuliza kama vile Mtu aliyetaka  kupata uthibitisho wa alichokisikia 

“Ndio, Martin Gimbo, unamfahamu?” Alihoji Mohd 

“Ndio, ni Mwanangu! Miaka mingi sasa tangia Martin  alipofariki kwa ajali ya gari akiwa anaelekea Mjini, tangu  siku hiyo sikuwahi kuamka na kukaa tena hata ongea yangu  ilikuwa ya shida, Martin alikuwa ndiyo Mwanangu wa pekee  niliyempenda, tumaini la Maisha yangu lilikuwa kwa Kijana wangu Martin baada ya Baba yake kufukiwa na kifusi huko  Merelani akiwa anafanya kazi za mgodi” Alisema Mama huyo,  kisha alimuomba Mjukuu wake amsindikize mahali. 

“Nifuateni” Alisema Mama huyo ambaye alijitambulisha kama  Mama yake Martin Gimbo ambaye alikuwa akitajwa kama gaidi  kiongozi wa kundi la ESS .

Nini Kitaendelea USIKOSE SEHEMU YA NNE

JIUNGE NA KIJIWENI WHATSAPP CHANNEL Kwa Kugusa Hapa 

Soma Riwaya Nyingine Za Kijiweni Kwa KUGUSA HAPA

Wewe kama MFANYABIASHARA.. Kuna wakati unatamani kuwafikia watu wengi zaidi na hujui wapi pa kuanzia , USIJALI kwani hapa ndipo ambapo MTAA UNAONGEA na tuko tayari kukusaidia kuwafikia watu wengi kwa BEI YA OFA

Njoo Utangaze Nasi Sasa Kwa Kutuambia Una TANGAZO Gani na unataka kutangaza kwa muda gani kwa kutuma ujumbe hapa WwhatsApp Kupitia Namba +255760871896 

16 Comments

  1. KingzJeelay on

    Wanaenda kufanywa nn… Kama ye ndo mkuu wa kitengo 🙆🏽‍♂️🙆🏽‍♂️🙆🏽‍♂️🥱🥱

Leave A Reply

Exit mobile version